Advertise here

Wednesday, March 13, 2013

WAJITOKEZA KUISAIDIA POLISI KIFO CHA PADRE ZANZIBAR

Zanzibar. Polisi imeanza kupokea majina ya watu wanaodaiwa kumuua Padri Evarist Mushi kutoka kwa wananchi, kutokana na mchoro uliotolewa unaoonyesha sura ya mtu anayedaiwa kumuua padri huyo.
Wananchi wamepiga simu polisi au kwenda kutoa majina ya watu wanaodhani wamefanana na mchoro wenye taswira ya mtu anayedaiwa kumuua Padri Mushi.
“Wametupigia simu na wengine wamekuja, kutwambia mtazameni fulani au fulani na sisi tunachunguza watu hao tuliotajiwa,” alisema Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mussa Ali Mussa.
Kamishna Mussa alisema mchoro huo umetolewa na Polisi Tanzania  wala siyo Askari wa Upelelezi wa Marekani (FBI), ambao wapo kusaidia kumsaka muuaji.
Kuhusu mchoro huo kumwonyesha mtu aliyevaa baraghashia, alisema kwa Zanzibar hilo ni vazi la utamaduni wala siyo la dini na  kwamba, anaweza kuwa alikuwa mtu kutoka Bara lakini alivaa hivyo ili kupoteza kufahamika.
Alisema uchunguzi mkali unaendelea, lakini hadi sasa hawajamnasa mtu ambaye wana ushahidi wa kutosha kumpeleka mahakamani.
Polisi juzi walitoa mchoro unaomwonyesha mtu anayedaiwa kumpiga risasi na kumuua Padri Mushi wa Kanisa Katoliki, Februari 17 mwaka huu.

No comments: