WAZIRI
wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe amesema kuwa atasitisha mikataba
yote ya magari yanayohusika kubeba mafuta na kusambaza katika Shirika la
Reli Tanzania (TRL) kutokana na hasara inayopatikana badala yake
kutumia usafiri wa shirika hilo.
Mwakyembe
alisema hayo mjini Morogoro alipofanya ziara ya kushtukiza kwenye
stesheni ya reli iliyopo mjini Morogoro na kudai kuwa hatakuwa tayari
kuendelea kufumbia macho suala hili la usafirishaji wa mafuta kwa magari
wakati shirika hilo lina uwezo wa kusafirisha mafuta kwa kutumia
usafiri wao.
Alisema
endapo shirika litatumia mabehewa yake kusafirishia mafuta shirika
halitapata hasara kama inayoendelea kupata kutokana na kutumia magari
binafsi kusambaza mafuta kwenye stesheni zote nchini. Kwa upande wa
wafanyakazi wa shirika hilo Kituo cha Morogoro, Taferi Dimisheni na
Ramadhani Dalueshi, walisema kuwa wanafanya kazi katika mazingira magumu
licha ya kuwa taifa linategemea pato kupitia shirika hilo.
Walisema
kumekuwa na tatizo la mabehewa ya mizigo kukaa muda mrefu kituoni hapo
kutokana na kukosekana kwa mafuta katika kituo hicho.
“Inafikia
wakati mafundi injini wanashindwa kutengeneza injini za treni kutokana
na kukosekana kwa mafuta na kusababisha msongamano wa mabehewa ambayo
yana mizigo ya wateja wao,” alisema Taferi
Kwa
upande wake, dereva wa treni inayofanya safari zake kati ya Dar es
Salaam na Morogoro, Rango Mboma alisema kuwa madereva wamekuwa wakifanya
kazi katika mazingira magumu hali inayowasababisha kuwa na madeni mengi
kutokana na kutegemewa na familia zao.
Alisema
kuwa kipato wanachopata wao hata dereva wa boda oda wanawazidi kwa
kipato hivyo Serikali inatakiwa kuwaboreshea masilahi wafanyakazi wa
kituo hicho.
Akitoa
ufafanuzi wa madai hayo Meneja wa Karakana ya Morogoro, Mhandisi Nejo
Ngosomwile alikiri kuwapo kwa matatizo hayo likiwamo la mafuta.
hivyo
kusababisha mabehewa ya mizigo kukaa kwa muda mrefu. Hivyo aliiomba
Serikali kuboresha masilahi ya wafanyakazi wakiwamo madereva kwani wao
ndiyo wanaotegemewa katika kusafirisha abiria.
No comments:
Post a Comment